Monday, May 14, 2012

  MAHAKAMA KUU KANDA YA ARUSHA YAAMURU WAKILI MWALE AREJESHEWE MAGARI YAKE.
 
 
WAKILI maarufu nchini,Median Mwale ameibwaga serikali katika rufaa iliyofunguliwa na mawakili wa serikali wakipinga uamuzi wa mahakama ya hakimu mfawidhi Arusha,iliyompa mamlaka  wakili huyo kurejeshewa  magari yake 7 ya kifahari yanayoshikiliwa katika ofisi za mamlaka ya mapato TRA mkoani Arusha.
Akisoma hukumu hiyo kwa zaidi ya saa 1,Jaji wa mahakama kuu kanda ya Arusha, Kakusulo Sambo alisema kuwa mahakama imetafakari kwa kina hoja za pande zote mbili na kubaini kuwa kimsingi rufaa iliyokuwa imefunguliwa na upande wa serikali ikiongozwa na mawakili wake,Neema Ringo na Fredrick Manyanda walikurupuka kwani hawakuwa wamesoma  vipengele vya sheria ipasavyo  ili kujiridhisha kabla ya kufungua rufaa hiyo.

Jaji Sambo alisema kuwa kati ya mapingamizi manne yaliyowekwa na wakili Mwale,pingamizi la pili lilidai kwamba ,maombi yaliyowasilishwa mahakamani na serikali ,hayana sifa ya kuwepo kwa kuwa yameletwa chini ya kifungu ambacho sicho na hakipo chini ya sheria zilizotungwa na bunge la jamhuri ya muungano Tanzania.

Alisema pingamizi hilo pekee lilitosha kutoa maamuzi madogo katika rufaa ya serikali,kwani lilibeba mapingamizi mengine yaliyobaki kutokana na uzito wa kipekee uliochukuliwa na mahakama . 

Awali alisema kuwa,maombi yaliyowasilishwa mahakamani hapo na mawakili wa serikali,Fredrick Manyanda na Neema Ringo juu ya kupinga maamuzi ya hakimu Charles Magesa wa mahakama ya hakimu mfawidhi,Arusha hayakuwa sahihi na yalijaa upungufu wa baadhi ya viambatanisho vinavyoweza kuishawishi mahakama  .

Jaji sambo alisisitiza kwa kuwataka mawakili wa serikali kusoma zaidi na kuvipitia mara kwa mara vifungu vya sheria na kuacha kukurupuka na kudai kuwa mawakili hao wamekuwa wakifanya makosa kama hilo mara kwa mara ,na mara nyingi amekuwa akiwasihi kupitia upya vifungu vya sheria kabla ya kuwasilisha shauri mahakamani.

Hata hivyo Jaji Sambo alitumia muda mwingi kutoa elimu kwa mawakili wa serikali,Neema Ringo na Fredrick Manyanga kuwa kifungu cha sheria namba 372 walichotumia kupeleka shauri hilo mahakama kuu ,hawakuwa wamekipitia na kukisoma vizuri ,kwani katika utetezi wao walidai kuwa kifungu hicho ni sahihi na kilihitaji madogo madogo.

Alisema kitendo cha mawakili hao wa serikali kudai kuwa kifungu hicho kilikosewa katika hatua ya uchapishaji ni hatari sana katika mwenendo mzima wa kesi,na hivyo mahakama haiwezi kutoa unafuu wowote  kwa kutumia kigezo hicho.

Jaji sambo baada  ya  hukumu hiyo aliamuru jalada hilo kurudishwa mara moja katika mahakama ya hakimu mkazi ili kuendelea na kesi ya msingi inayomkabili wakili Mwale.

Awali mawakili hao wa serikali  walikata rufaa Mahakama Kuu wakitaka  ipitie upya maamuzi yaliyofanywa na mahakama hiyo iliyotoa maamuzi ya magari hayo kukabidhiwa wakili Mwale.

Uamuzi huo ulitolewa na  Hakimu Mkazi Mfawidhi  Magesa, ambaye alisema baada ya kupitia ushahidi wa pande zote, mahakama yake imeridhika kuwa mamlaka hizo zilikamata magari hayo kinyume cha sheria ya matunda ya uhalifu (Proceeds Crimes Act) pamoja na vifungu namba 41 na 44 vya sheria ya mwenendo wa kesi za jinai.

Magari yaliyoamriwa na mahakama kurejeshwa kwa Mwale ni T 690 BEW aina ya Range Rover, T 643 BTS Land Rover Discovery, T 907 BTS BMW, T 118 BRS Cadillac Escalade, T 499 APX Land Cruiser, T 520 BBJ BMW, ambayo yalichukuliwa Novemba mosi, pamoja na gari  T 660 BCG Toyota Chaser lililokamatwa Desemba 8, mwaka jana.

No comments:

Post a Comment