Tuesday, May 29, 2012

      MONDULI WATAKA KATIBA MPYA

MWENYEKITI WA UVCCM, MONDULI, JUILUS KALANGA WANANCHI wa Monduli wametakiwa kujitokeza kwenye mikutano ya kukusanya maoni ya katiba mpya ili waweze kutoa mapendekezo yatakayowawezesha kunufaika na rasilimali zao ikiwemo misitu na mapori yanayotumika kwa utalii wa kuwinda.
Hayo yalisemwa na mwenyekiti wa Umoja wa vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) wilayani humo, Julius Kalanga wakati alipokuwa akiwaeleza waandishi wa habari maazimio ya kikao cha kamati ya utekelezaji kilichokaa mwishoni mwa wiki .
 Alisema kuwa wilaya hiyo ina misitu na vitalu vya uwindaji wa kitalii lakini wananchi wake hawanufaiki navyo kwani malipo yote hufanyikia wizarani jambo alilosema kuwa si sahihi kwani wananchi wanaoishi kuzunguka maeneo hayo ambao huwa walinzi na hupata athari mbalimbali ikiwemo wanyama kuvamia mashamba na makazi yao hivyo wanapaswa kupata sehemu ya mapato. 
Kalanga ambaye pia ni diwani wa Nyampulukano alisema kuwa tatizo hilo linaweza kutatuliwa kwa wananchi kujitokeza kwenye mikutano ya kukusanya maoni ya katiba mpya ambapo alishauri angalau asilimia 25 mpaka 30 ya mapato ya uwindaji wa kitalii na uvunaji wa miti kwa ajili ya mbao yakarudishwa kwa jamii zinazoishi kwenye maeneo kuzunguka vitalu vya uwindaji na mazao ya misitu. 
 Aidha Mwenyekiti huyo wa UVCCM alisema kuwa wanamshukuru mbunge wao, Edward lowassa kwa kuamua kuweka wazi msimamo wake wa kutokihama chama hicho tawala kwani kabla ya hapo kulitokea sintofahamu kubwa miongoni mwa wanaCCM ambao wengine walitaka kukihama chama hicho wawahi kule ambapo waliambiwa mbunge wao atahamia.
 Pia walimpongeza Lowassa kwa kufanikiwa kutatua kero za ardhi kati ya wawekezaji na wananchi wa maeneo ya Mto wa Mbu na Meserani kwa kile alichoeleza kuwa endapo asingefanya haraka kutafutia ufumbuzi ingesababisha wananchi wengi kukikimbia chama hicho tawala. 
 “Kama wananchi wakiona hawawezi kupata haki ndani ya chama chao (CCM) watatafuta mahali pengine kwa kuipata nje ya chama chao hivyo tunamshukuru Lowassa kwa kuamua kuishughulikia migogoro hiyo ya ardhi na ufumbuzi alioupatia jambo lililosababisha wananchi kutulia” alisema kalanga.
KATIBU WA UVCCM MONDULI, EZEKIEL MOLLEL. 
 Kwa upande wake katibu wa UVCCM wilayani humo, Ezekiel Mollel alisema kuwa uchaguzi ndani ya chama hicho umeshindwa kukamilika kwenye baadhi ya maeneo kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ile ya baadhi ya watendaji wa chama kutotoa fomu za kugombea huku kwenye maeneno mengine akijitokeza mgombea mmoja.
 Alisema kuwa hali hiyo imepelekea mashina 497 kati ya 2,106 wilayani humo kutofanya uchaguzi na matawi nane kati ya 72 kushindwa kufanya uchaguzi huo ambapo kwa sasa mchakato wa uchaguzi ngazi ya kata unaendelea kwa wanaCCM kuendea kuchukua fomu.
Habari na Grace Macha.

No comments:

Post a Comment